Friday, September 4, 2015

TFF YAMTOSA ZITTO KABWE MECHI YA STARS VS NIGERIA

Zitto Kabwe
Na Bertha Lumala, Dar es Salaam 
WAKATI kiongozi wa Chama cha ACT Wazendo, Zitto Kabwe, ameomba Watanzania waruhusiwe kuingia bure uwanjani kuishangilia Taifa Stars dhidi ya Nigeria keshokutwa Jumamosi, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limetangaza viingilio vikubwa kwa ajili ya mechi hiyo ya kuwania kufuzu fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON) 2017. 
Wakati wa uzinduzi wa kampeni za chama hicho kuhusu uchaguzi mkuu mwaka huu zilizofanyika Mbagala jijini Dar es Salaam Jumapili, Zitto alishauri TFF iruhusu mashabiki waingie bure kwenye Uwanja wa Taifa kuipa sapoti kubwa timu ya nyumbani. 
Hata hivyo, katika mkutano na waandishi wa habari kwenye ofisi za TFF jijini Dar es Salaam leo, Baraka Kizuguto, ofisa habari na mawasiliano wa shirikisho hilo, ametangaza kiingilio cha chini ya Sh 7,000 huku akimjibu kwa kifupi Zitto kwa kusema: “Tusichanganye siasa na michezo”. 
Kizuguto amesema maandalizi ya mechi hiyo ya Kundi G yamekamilika huku akieleza kuwa kiingilio cha juu (VIP A) Sh 40,000, VIP B Sh 30,000, VIP C Sh15,000, Rangi ya Machungwa Sh 10,000 wakati viti vya rangi ya Bluu na Kijani Sh 7,000. 
Amesema tiketi za mchezo huo zinatarajiwa kuanza kuuzwa leo saa 4 asubuhi katika vituo 10; Ofisi za TFF, Buguruni, Mbagala, Ubungo, Makumbusho, Uwanja wa Taifa, Mwenge, Kivukoni, Posta (Luther House) na Kariakoo (Msimbazi). 
Amesema mechi hiyo itakayoanza saa 10:30 jioni kwa saa za Afrika Mashariki, itachezeshwa na waamuzi kutoka Rwanda ambao wanatarajiwa kuwasili jijini leo jioni. 
Marefa hao ni Louis Hakizimana (kati), Honore Simba (msaidizi), Jean Bosco Niyitegeka (msaidizi) na Abdoul Karim Twagiramukiza (wa akiba) pamoja na kamisaaa Charles Kasembe kutoka Uganda.

No comments:

Post a Comment

Popular Posts