Saturday, August 29, 2015

MAN CITY AKUTANA NA WABABE HAWA TENA

Manchester City logo
Na Salym Juma
Asee haya mataifa ya Ulaya yananifurahisha sana eti leo yanalalamika kuhusu wimbi la wahamiaji haramu kupitia Libya wakati wao ndio chanzo cha haya yote. Muammar Gaddafi alipokuwa imara ni nani aliyekatiza Libya kuingia Ulaya kirahisi? Tena bado tegemeeni pia wahamiaji wengine kibao kutoka Yemen na Syria maana nyie ndo chanzo cha yanayoendelea Mashariki ya Kati. Eti unakuta nchi ya Amerika na Ulaya zinaoongoza kuuza mafuta, jiulize wanatoa wapi? Ugaidi duniani kuisha ni ngumu sana maana kuna mambo kibao yaliyojificha zaidi hata ya zile chaguzi za DRFA. Anyway tugeukie kwenye soka maana binafsi napata hasira sana nikizitazama sera za nje za mataifa ya Magharibi.
Katikati ya wiki hii macho na masikio mengi yalielekea pale Monaco, sehemu ambapo ‘Draw’ ya kupanga makundi nane yenye timu 32 ilikuwa inafanyika, mbali na mchawi Messi kutajwa kama mchezaji bora wa Ulaya kwa mara ya pili, kitu kingine kilichoteka watu ni kitendo cha kundi la D kuwa na timu zenye msimu mzuri ama kwa lugha ya vijana wanasema zipo‘Onfire’. Kundi hili lina timu za Juventus, Manchester City, Sevilla na ndugu zangu Borussia Monchengladbach. Kwa wale wapenzi wa soka, kundi hili sio la kifo bali ni zaidi ya kifo. Naamini yapo mengi ya kutazama juu ya kundi hili.
Kwa wale ndugu zangu ambao tunapoteza muda wetu mwingi kufuatilia habari za michezo hususani soka, mtaungana na mimi kuwa tangu waarabu wamwage pesa pale Etihadi, Man City ilirejea kwenye michuano ya Ulaya ila imekuwa ikikwamishwa na timu kutoka mataifa matatu, Hispania, Ujerumani na Italia. Msimu huu pia City imekutana na timu kutoka mataifa haya kwenye hatua za mapema kabisa. Ungana nami hadi mwisho wa makala hii kutathmini kundi hili hatari kabisa pengine kuliko makundi mengine saba. Karibu sana…..
Manchester City baada ya uwekezaji wa kutosha tangu kuondoka kwa Mark Hughes, City ilifika fainali ya kwanza tangu miaka 30 kupita kwa kuchea fainali ya FA mwaka 2011. Kwa mara ya kwanza tangu 1968, City ilirejea kwenye ligi ya mabingwa barani Ulaya mwaka 2011 na kujikuta inapangwa na Bayern Munich, Villarreal na Napoli. Man City walishindwa kuifunga Napoli kwenye mechi ya ufunguzi na hatimaye baada ya vipigo kutoka kwa Napoli na Bayern Munich, City walishika nafasi ya 3 baada ya Villarreal kuonekana vibonde na hii ndo ilikuwa safari ya mwisho ya City kwenye makundi.
Msimuu wa 2012-13, Manchester City kama ilivyo kawaida ilikutana tena na Wajerumani na Wahispania japokuwa safari hii Wataliano hawakuwepo. Real Madrid na Borussia Dotmund walipangwa kundi moja na City huku Ajax akifunga hesabu ya kundi. Man City ilionewa sana kipindi hiki kwani hata nafasi ya kucheza Europe league hawakuipata baada ya kushika mkia nyuma ya Ajax. City hawakushinda mechi hata moja licha ya kuwa wababe kwenye Epl kwa kipindi hiki, walitoa sare tatu huku wakipoteza mara tatu na kuruhusu magoli ya kutosha.
Msimu wa 2013-14, mzimu wa Kijerumani ulizidi kuwaandama City kwa mara nyingine hasa baada ya kupangwa tena na Wajerumani. Kipindi hiki walipangwa na Bayern Munich huku Victoria Plzen na CSKA Moscow wakikamilisha kundi. City ilijitahidi baada ya kuwaonea vibonde hawa wawili na hatimaye kumaliza nyuma ya Bayern baada ya kutoa vipigo vitano na kupoteza mara moja. Mzimu wa Kihispania haukuwaacha City kwani walipata kipigo kitakatifu cha 4-1 na kutolewa na FC Barcelona kwenye hatua ya 16 bora. Hapo Wahispania na Wajerumani waliikwamisha tena City.
Msimu uliopita City walikutana tena na Wajerumani na Waitaliano. Bayern Munich na AS Roma ndio timu zilizoingia kwenye kundi moja na City huku CSKA Moscow wakikamilisha kundi la nne. City walifanya upuuzi sana japokuwa walifuzu 16 bora kwani walishinda mechi mbili pekee huku wapinzani wao Roma na CSKA wakishinda mechi moja moja. Kama kawaida Wahispania waliwakwamisha tena City baada ya Barcelona kuwatoa kwenye raundi ya 16 bora kwa jumla ya magoli 3-1. Ukijaribu kutazama safari yao tangu kurejea kwenye UEFA wamekuwa wakikwamishwa na Wajerumani, Wataliano na Wahispania.
Juventus ni timu nyingine ya Italia ambayo imepangwa na City msimu huu. Juventus ni mabingwa wa Italia na makamu bingwa pia wa Kombe hili. Ukijaribu kukiangalia kikosi cha Juventus licha ya kuondokewa na wachezaji wake muhimu ila kuna kitu kimoja kinaitwa ‘uzoefu’ wa michuano ya Ulaya. Juve ni miongoni mwa timu zenye vikosi vipana kidogo pale Italia tofauti na timu nyingine, kutokana na hili usishangae ikachukua pointi 4 kwenye mechi 2 itakazo kutana na Man City. Wengi tunajua kuwa City ni wazuri ndani ila nje ni wa kawaida sana na hili litazidi kutokea tena. 
FC Sevilla ni timu nyingine iliyopangwa na City kundi moja. Kumbuka hawa ni mabingwa wa Europe league na shughuli yao Barcelona wanaijua.Nitakuona wa ajabu kama ukiniambia City itachukua pointi yoyote pale Estadio Ramon Sanchez Pizjuan watakapokutana na FC Sevilla. Hata pale watakapoikaribisha Etihad bado itakuwa ngumu kuwafunga Wahispania hawa ambao wamekuwa tishio kubwa sana kwa timu za Barcelona na Real Madrid kwenye La liga. Sevilla wapo vizuri sana wanapokutana na timu za kizembe na usishangae kuona wanachukua nafasi 2 za juu kwenye kundi hili gumu.
Wajerumani wengine watakao ongeza gundu kwa City ni Borussia Monchengladbach, vijana wa pale Stadionim Borussia Park chini ya kocha wao Lucien Favre. Monchengladbach walimaliza nafasi ya tatu kwenye ligi ngumu ya Bundesliga msimu uliopita. Walitolewa kwenye hatua za awali za michuano ya Europe league msimu uliopita ila shughuli yao ilionekana kwenye Bundesliga. Msimu huu wameanza vibaya baada ya kikosi chao kutotulia ila bado itakuwa sio kazi rahisi kwa City kuchukua pointi pale Ujerumani mbele ya mashabiki 54, 000 wa Monchenglabach. Inawezekana Monchengladbach ikapoteza mechi nyingi za ugenini kutokana na kutokuwa wazuri nje ya Ujerumani ila kwa mechi tatu za ndani isipoteze mechi hata moja.
Kwa ujumla mbinu mbadala za Manuel Pellagrin na kuwaandaa wachezaji wake Kisaikolojia ndicho kitu ambacho kinaweza kuwasaidia kumaliza kwenye nafasi mbili za juu katika kundi hili la kifo. Juventus kwenda kuchukua pointi moja Hispania, moja Ujerumani na ttu pale Etihad ni kitu cha kawaida sana kama City hawatojipanga vizuri. Pia Sevilla kwenda kuchukua pointi moja pale Etihad na tatu Ujerumani ni kitu cha kawaida kabisa. Bila shaka City inapaswa kushinda mechi zote za nyumbani au hata kukusanya pointi saba kati zile tisa za nyumbani, wakifanya hivi watakuwa wamemaliza kazi mapema sana.
Mwisho wa siku japokuwa soka ni mchezo wa makosa na huwezi kutabiri mpira wa miguu kwani maajabu yana nafasi yake ila inawezekana kundi hili likamtoa mshindi wa kwanza akiwa na pungufu ya pointi 12 huku magoli ya kufunga na kufungwa yakiamua nani asonge mbele nani abaki Europe league na nani ashike mkia. Manueli Pelagrin anapaswa kuchanga karata zake vyema ili asije kuaibika kwa mara nyingine tena kwenye michuano hii mikubwa kabisa katika ngazi ya Ulaya barani Ulaya. Yetu macho tuu na ‘Inshaa Allah’ tutajaaliwa uzima na kushuhudia kila kitu kwenye kundi hili.

No comments:

Post a Comment

Popular Posts